EADB na UN Rwanda waungana kusaidia SMEs, vijana na wanawake wajasiriamali

Share Now

Na Christopher Karenzi

chriskarenzi @gmail.com

Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) na UN Rwanda zimesaini makubaliano ya kusaidia Biashara Ndogo na za Kati (SMEs), hususan za vijana na wanawake nchini Rwanda. Hafla hii ilifanyika jijini  Kigali, Machi 26, 2026

Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) na Umoja wa Mataifa nchini Rwanda (UN Rwanda) wamesaini Hati ya Makubaliano (MOU) yenye lengo la kusaidia Biashara Ndogo na za Kati (SMEs), vijana pamoja na wanawake wajasiriamali nchini Rwanda.

Ushirikiano huo unalenga kuboresha upatikanaji wa fedha, kuimarisha ujuzi wa ujasiriamali na kukuza ubunifu, ili kuchochea ukuaji wa uchumi na ajira. Pia unatarajiwa kuondoa changamoto kama ukosefu wa mitaji na ujuzi, huku ukipanua fursa za kiuchumi kwa makundi mbalimbali.

Mkurugenzi Mkuu wa  EADB, Benard Mono 

Akihutubia waliohudhuria kikao  kwa niaba ya Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB), Mkurugenzi Mkuu wa  EADB, Benard Mono  amesema kwamba amefarijika  jinsi wanavoshirikiana bega kwa bega na mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini Rwanda, ‘’Nimefarijika sana kuwa tumekutana katika mazingira haya ili kutafakari si tu mafanikio yetu ya pamoja, bali pia ushirikiano unaoendelea kuunda mustakabali wetu’’.

‘’Jioni ya leo, ningependa kwa ufupi kuangazia ushirikiano wetu na mashirika ya Umoja wa Mataifa hapa Rwanda, unaolenga kusaidia Biashara ndogo ndogo na za kati (SMEs), ambazo zinaendelea kuwa uti wa mgongo wa uchumi wetu’’ Ameongeza

Katika Hotuba yake  Dkt. Fatmata Lovetta Sesay, Kaimu Mratibu wa Umoja wa mataifa (UN) amesema kwamba,  hili si tukio la kusaini tu, bali ni dhamira ya pamoja ya kufungua na kuendeleza uwezo wa Biashara ndogo na za kati (SMEs), vijana na wanawake wajasiriamali nchini Rwanda.

Amesema: ‘’Lengo letu liko wazi. Tunakusudia kuharakisha maendeleo ya Biashara ndogo na za Kati (SMEs), kukuza ujasiriamali wa vijana, na kuwawezesha wanawake kuongeza idadi ya kufanya biashara. Kwa pamoja, tutabuni na kuanzisha bidhaa za kifedha zinazolengwa kulingana na mahitaji, ikiwemo mikopo yenye masharti nafuu, mifumo ya ufadhili mchanganyiko, dhamana, na uwekezaji wa hisa’’.

Dkt. Fatmata Lovetta Sesay, Kaimu Mratibu wa Umoja wa mataifa (UN)

Aidha amesema  lengo lao  la pamoja ni kuimarisha mazingira ya Rwanda kwa ajili ya ukuaji wa uchumi endelevu na shirikishi, kutoa  msaada wa kiufundi, kuwezesha ubadilishanaji wa maarifa, na kujenga ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi, taasisi za elimu, pamoja na vituo vya ubunifu.

Tangu Agosti 2024, UN Rwanda imekuwa ikishirikiana na EADB, ikijenga juu ya programu ya EADB inayosaidia zaidi ya SMEs 500 katika sekta za kilimo, biashara, usafirishaji na viwanda.

Nchini Rwanda, SMEs zina nafasi muhimu katika uundaji wa ajira, ubunifu na ukuaji jumuishi. Hata hivyo, mara nyingi hukumbana na changamoto zinazoendelea kuwepo, hususan katika upatikanaji wa fedha, ujenzi wa uwezo, na upatikanaji wa masoko. Vikwazo hivi havizuizi tu ukuaji wao, bali pia mchango wao mpana katika mageuzi ya kiuchumi.

Ushirikiano wetu na mashirika ya UN umeundwa kushughulikia mapungufu haya kwa njia iliyoratibiwa na yenye matokeo chanya zaidi. Kwa kuunganisha nguvu za UN katika utaalamu wa kiufundi, ujenzi wa uwezo na maendeleo ya kijamii, pamoja na jukumu la EADB kama taasisi ya fedha za maendeleo, tunaunda mfumo jumuishi zaidi wa kusaidia SMEs.

Kupitia ushirikiano huu, tunafanya kazi kupanua upatikanaji wa huduma za kifedha zinazolengwa, kuimarisha ujuzi wa ujasiriamali, na kusaidia ubunifu—hasa kwa biashara zinazoongozwa na vijana na wanawake. Wakati huohuo, tunasaidia SMEs kujiunganisha na minyororo ya thamani, ili ziweze kukua na kushindana kwa ufanisi zaidi katika ngazi ya kikanda na kimataifa. Ushirikiano huo unatarajiwa kuyawezesha mashirika hayo mawili kuunganisha nguvu zao ili kuharakisha ukuaji wa SMEs nchini humo.

Mkurugenzi Mkuu wa EADB, Bw. Benard Mono (kushoto),na Kaimu Mratibu wa UN Rwanda, Dkt. Fatmata Lovetta Sesay, wakionesha nakala zao za makubaliano yaliyosainiwa.

Kupitia makubaliano hayo, taasisi hizo zinalenga kuunda mazingira rafiki yatakayochochea ukuaji na uendelevu wa SMEs, ambazo zina mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa Rwanda. Pia ushirikiano huo utatumia utaalamu wa kifedha wa EADB pamoja na utaalamu wa kiufundi na uwezo wa UN katika kuhamasisha rasilimali zinazohitajika kwa maendeleo ya SMEs.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa EADB, Benard Mono, alisema kuwa kwa kuunganisha nguvu za UN katika utoaji wa utaalamu wa kiufundi, ujenzi wa uwezo na maendeleo ya kijamii, pamoja na jukumu la EADB kama taasisi ya fedha za maendeleo, wanakusudia kupanua upatikanaji wa huduma za kifedha zinazolengwa, kuimarisha ujuzi wa ujasiriamali na kusaidia ubunifu, hususan kwa vijana na wanawake. Aliongeza kuwa juhudi hizo pia zinalenga kushughulikia changamoto zinazoikabili sekta ya SMEs, ikiwemo upatikanaji wa mitaji na ujenzi wa uwezo.

Kwa upande wake, Mratibu Mkazi wa UN Rwanda, Dkt. Fatmata Lovetta Sesay, alisema ushirikiano huo unatarajiwa kufungua fursa muhimu za upatikanaji wa fedha na msaada wa kiufundi ambao UN kwa kushirikiana na EADB na wadau wengine inaweza kuhamasisha kwa ufanisi. Alieleza kuwa mpango huo utalenga kuondoa vikwazo vya kimfumo vinavyozuia upatikanaji wa fedha, ujuzi na masoko, hasa kwa wanawake vijana na makundi yaliyo hatarini.

Kwa ujumla, ushirikiano huo unatarajiwa kuchangia katika uundaji wa ajira, kuimarisha ukuaji na uendelevu wa SMEs, pamoja na kupanua fursa za kiuchumi kwa kiwango kikubwa.Makubaliano hayo pia yanatambua umuhimu wa SMEs kama injini ya ukuaji wa uchumi, na yanalenga kuharakisha maendeleo ya sekta hiyo, kukuza ujasiriamali kwa vijana na kuwawezesha wanawake wanaoongoza biashara nchini Rwanda.

EADB ni nini hsa?

The East African Development Bank  (EADB), ni Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) ilianzishwa mwaka 1967 chini ya mkataba wa iliyokuwa Jumuiya ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Dhamira yake ilikuwa kutoa msaada wa kifedha na huduma zinazohusiana kwa mashirika katika nchi wanachama, ambayo kupitia shughuli zao yangetoa mchango chanya katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya ukanda.

Benki hiyo ilianzishwa upya mwaka 1980 chini ya Hati mpya. Kupitia Hati hiyo, jukumu na dhamira yake vilipitiwa upya na wigo wa shughuli zake kupanuliwa ili kujumuisha huduma mbalimbali za kifedha katika nchi wanachama, ikiwa na lengo kuu la kuimarisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi pamoja na ushirikiano wa kikanda.

Kwa sasa, EADB inamilikiwa na nchi nne wanachama ambazo ni Kenya, Uganda, Tanzania na Rwanda, pamoja na taasisi nyingine za maendeleo na za kifedha za kibiashara.

Kama chombo cha Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), na kupitia ushirikiano wake na taasisi za EAC, benki hiyo imepata jukwaa la kuchochea kwa kiasi kikubwa mchakato wa ujumuishaji wa kikanda kwa kutoa huduma za fedha za maendeleo.


Share Now

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *